Ripoti ya Glass House Brand Trust 2025, imeonyesha kuwa Tanzania imezishinda nchi zote za Afrika Mashariki na kuwa chaguo kuu kwa Wakenya wanaotaka kuhamia nchi jirani. Utafiti huo, uliotathmini kiwango cha imani kati ya watumiaji Wakenya na taasisi mbalimbali, umeonyesha kuwa asilimia 35.25% ya waliichagua Tanzania kuliko mataifa mengine ya Afrika Mashariki, wakitaja utulivu, gharama nafuu za maisha, na ukaribu wa kitamaduni kama sababu kuu. Ripoti hii inatoa mwanga muhimu kuhusu mabadiliko ya mtazamo nchini Kenya na mwenendo mpana wa uhamaji wa kikanda unaoweza kubadili mustakabali wa utalii na usafiri Afrika Mashariki.
Sababu Zinazowavutia Wakenya kuhamia Tanzania
Wakenya wameonyesha kuvutiwa zaidi na Tanzania kutokana na sababu kadhaa muhimu. Ya kwanza ni kiwango cha chini cha rushwa, ambapo asilimia 15% ya washiriki walitaja hili kama sababu kuu ya kuchagua kuhamia Tanzania. Uwazi na utawala bora vinaendelea kuwa vipaumbele kwa wanaofikiria kuhamia nchi jirani, na Tanzania inaonekana kuwa mbadala thabiti ukilinganisha na changamoto za rushwa zilizokithiri nchini Kenya.
Mbali na utawala, gharama nafuu za maisha zimetajwa kwa kiwango kikubwa, ambapo 14.5% walieleza kuwa ndiyo sababu ya kuvutiwa kwao na Tanzania. Utulivu wa kiuchumi pia umeonekana kuwa sababu muhimu, kwa kuwa 14% ya waliohojiwa wana imani na kasi ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania na uwezo wake wa kustawi zaidi siku zijazo.
Usalama na ukaribu wa kitamaduni pia vilitajwa. Asilimia 11.5% ya washiriki walitaja usalama kama sababu ya msingi ya uamuzi wao, wakisisitiza sifa ya Tanzania kama nchi yenye amani. Zaidi ya hapo, 11% waliona ukaribu wa kitamaduni na urithi wa Afrika Mashariki kama kivutio kikubwa kwao.
Sababu za mtindo wa maisha kama uwiano wa kazi na maisha na mazingira mazuri vilichangia kuwavutia, ingawa kwa kiwango cha kati. Fursa za ajira (6%) na miundombinu (5.75%) zilitajwa kwa viwango vya chini lakini bado ni sehemu ya vigezo vya kufanya uamuzi.
Rwanda na Uganda: Nafasi ya Pili na ya Tatu
Wakati Tanzania ikishika nafasi ya kwanza, Rwanda na Uganda zinafuatia. Rwanda, inayosifika kwa utawala bora, usafi na usalama, ilipendekezwa na 31.5% ya Wakenya. Mageuzi yake makubwa katika utawala na miundombinu yameifanya kuwa moja ya nchi salama zaidi, hivyo kuvutia wahamiaji kutoka Kenya.
Uganda ilishika nafasi ya tatu kwa 20% ya waliohojiwa, ikivutia kutokana na utamaduni hai na ukaribu wake na Kenya. Hata hivyo, wasiwasi wa kisiasa umepunguza mvuto wake ikilinganishwa na Rwanda na Tanzania.
Changamoto za Kenya: Rushwa na Gharama za Maisha
Ingawa Tanzania, Rwanda na Uganda zinawavutia Wakenya wanaotafuta fursa mpya, sababu za kutoridhika na Kenya ziko wazi. Takriban 29% ya washiriki walitaja rushwa kama tatizo sugu linalopunguza ufanisi wa huduma za umma, kuongeza gharama, na kudhoofisha imani kwa taasisi.
Gharama za juu za maisha zilitajwa na 23%, huku mfumuko wa bei na ongezeko la matumizi ya kaya vikisababisha wengi kutafuta maisha nafuu nje ya nchi. Jiji la Nairobi limetajwa kama eneo lenye gharama kubwa zaidi.
Huduma za afya, zilizotajwa na 21.25%, ni chanzo kingine cha malalamiko, kutokana na gharama kubwa, upungufu wa wahudumu na muda mrefu wa kusubiri.
Masuala ya usalama na ukosefu wa polisi wa kutosha yalitajwa na 13.5% ya washiriki, sambamba na kutoridhishwa na utawala, ambapo 14.5% walitaja ukosefu wa uwajibikaji na ulegevu katika mageuzi.
Mwelekeo Mpya wa Uhamaji na Athari kwa Utalii wa Kikanda
Matokeo ya ripoti ya mwaka huu yanaonyesha mabadiliko makubwa kwenye chaguo za Wakenya na mwenendo wa uhamaji Afrika Mashariki. Huku Wakenya wengi wakifikiria kuhamia nchi jirani, ni wazi kuwa utawala bora, gharama nafuu na utulivu vinazidi kuwa vigezo muhimu.
Kwa sekta ya utalii, hii inatoa mwongozo muhimu kuhusu maeneo ya kuwekeza. Tanzania, Rwanda na Uganda zinatarajiwa kuona ongezeko la wahamiaji na watalii kutoka Kenya kwa kuwa zinaendelea kuboresha uchumi, usalama na utawala.
Kenya wana la kujifunza: Nafasi ya Mageuzi na Maendeleo
Matokeo haya ni wito kwa Kenya kuchukua hatua. Wingi wa Wakenya wanaotaka kuhama kutokana na rushwa, gharama za juu za maisha na changamoto za afya zinaonyesha umuhimu wa mageuzi ya haraka. Serikali inapaswa kutatua chanzo cha matatizo haya ili kuzuia upotevu wa rasilimali watu kwa nchi jirani.
Ili Kenya ibaki kuwa taifa lenye ushindani, ni lazima ishughulikie masuala ya utawala, kupunguza gharama za maisha, na kuboresha huduma za umma, hasa afya na usalama. Pia kuna fursa ya kuboresha sekta ya utalii ili kuvutia wageni zaidi.
Ripoti ya Glass House Brand Trust 2025 inatoa taswira muhimu ya mustakabali wa uhamaji na utalii Afrika Mashariki. Kadri Tanzania na Rwanda zinavyoendelea kuvutia Wakenya zaidi, Kenya inahitaji kukabiliana na changamoto za ndani ili kubaki na nafasi yake ya uongozi wa kikanda.
Katika miaka ijayo, kupanda kwa hadhi ya Tanzania kama chaguo kuu kwa Wakenya kunaweza kubadili mienendo ya kikanda. Namna Kenya itakavyojibu changamoto hizi ndiyo itakayoamua nafasi yake katika ushindani wa Afrika Mashariki.
